Wakati vijana 40,000 wenye umri kati ya miaka 15 hadi 24, wakibainika kuambukizwa ugonjwa wa Ukimwi jijini Dar es Salaam, viongozi, wabunge na wafanyabiashara wametajwa kuwa vinara wa kusambaza ugonjwa huo.
Mratibu wa Vijana wa Tume ya Taifa ya Kudhibiti
Ukimwi (Tacaids), Grace Kessy akizungumza katika warsha ya siku nne ya
wawakilishi wa mashirika ya vijana yanayojihusisha na vita dhidi ya
Ukimwi nchini jijini hapa alisema, vijana wasipobadili tabia wataendelea
kuwapo hatarini.
Alisema katika taarifa zilizokusanywa mwaka 2011
hadi 2012 ilibainika kuwa, kati ya vijana waliopimwa 40,000 walikuwa na
maambukizi Dar es Salaam, wakifuatiwa na vijana 10,000 kutoka mikoa ya
Shinyanga, Kagera na Mbeya.
“Tatizo la maambukizi ya Ukimwi ni kubwa hasa kwa
vijana hivyo ni muhimu kuwa na mikakati ya pamoja kudhibiti hali hii,”
alisema.
Mbunge wa Jimbo la Arusha, Godbless Lema akifungua
warsha hiyo alisema, suala la kuendelea kuenea kwa Ukimwi ni la
kimaadili kwani sasa wanaoharibu watoto ni watu wenye uwezo, wakiwamo
wabunge, wafanyabiashara na viongozi kutokana na umaskini wa vijana.
“Taifa lina tatizo kubwa la kimaadili hivi sasa
wazazi wameacha jukumu la kulea watoto na kuachiwa wafanyakazi wa ndani,
mitandao ya kijamii na simu za mkononi,” alisema.
Alisema ili Taifa lishinde vita hiyo, ni muhimu
mashirika hayo kuongeza jitihada za kulinda maadili katika jamii, kupiga
vita umaskini na utumiaji wa pombe ovyo kwa kushirikiana na watungaji
wa sera.
Awali, mratibu wa mafunzo hayo yaliyoandaliwa na
Mtandao wa Mashirika ya Kupambana na HIV katika Ukanda wa Afrika ya
Mashariki, Jovinniah Mollel alisema, vijana kwa sasa wapo hatarini zaidi
katika vita dhidi ya Ukimwi.