Saa chache baada ya Dk John Magufuli kutangazwa kuwa mteule wa CCM kuwania urais, ulinzi umeimarishwa kwa mgombea mwenyewe, nyumbani kwake eneo la Ada Estate, Dar es Salaam na jimboni Chato mkoani Geita.
Muda mfupi baada ya kuwapo taarifa kuwa Magufuli
anaongoza kura za wajumbe wa Mkutano Mkuu, aliongezewa ulinzi usiku huo
na hadi jana muda wote, alionekana akiwa na walinzi watano.
Jimboni Chato, nyumbani kwake eneo la Rubambambangwe, polisi walionekana wakitanda tangu jana asubuhi tofauti na siku nyingine.
Askari hao wakiongozwa na Mkuu wa Polisi Wilaya ya
Chato, Alex Mkama walionekana nyumbani hapo tangu asubuhi hata kabla
matokeo yaliyompa ushindi Dk Magufuli hayajatangazwa.
Mwandishi wa habari hizi ambaye alikwenda nyumbani
kwa Dk Magufuli kuzungumza familia yake, hakuruhusiwa na polisi
waliokuwa kwenye lango kuu la kuingilia, walidai wamepewa maelekezo ya
kutoruhusu watu kuingia.
“Naomba usiingie ndani wala kupiga picha eneo
hili, hayo ndiyo maelekezo ninayokupa na niliyopewa, vinginevyo mtafute
RPC (Kamanda wa Polisi Mkoa) akupe ruhusa,” alisema mmoja wa askari hao.
Akizungumzia hali hiyo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita, Joseph Konyo
alisema polisi walikuwa wanatekeleza jukumu lao kwa umma la kulinda raia
na mali zao kutokana na wananchi kwa makundi kusherehekea ushindi wa
mteule huyo.
Konyo alisema ulinzi huo ulilenga kuweka na kuimarisha usalama kwenye makazi ya familia hiyo.
Hata hivyo, Konyo alipotakiwa kuzungumzia kuzuia
watu kupiga picha kwenye makazi hayo alikata simu na hata alipopigiwa
tena hakupokea.
Nyumbani kwake, Ada Estate, ulinzi ulianza
kuimarishwa mara tu baada ya kiongozi huyo kutangazwa kuwa mgombea wa
urais kupitia CCM.
Mmoja wa walinzi hao ambaye hakutaka kutaja jina
lake alisema wameongezwa walinzi wengine wanne mara baada ya matokeo ya
mjini Dodoma kutangazwa.
Magari kadhaa yenye namba za serikali na magari ya polisi yalionekana yakiingia na kutoka nyumbani kwa Magufuli.
Kadhalika kama ilivyokuwa Chato, walinzi hao
walisema wamepewa amri kutoruhusu watoto au mwanafamilia yeyote kutoka
nje au kuzungumza na waandishi wa habari.