Header ads

Header ads
» » Bilal Amemtuma Lowassa Kuongoza Harambee ya Kuchangia Ujenzi wa Msikiti wa Patandi Mkoani Arusha:


Wakati CCM ikifanya jitihada za kudhibiti makada wake wanaotajwa kuwania urais, Makamu wa Rais, Dk Mohamed Gharib Bilal amemtuma waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa kuendesha moja ya shughuli ambazo chama hicho kinaamini kuwa ni moja ya majukwaa ya kampeni kwa wagombea.
Dk Bilal amemtuma Lowassa, mmoja wa makada wanaotajwa kutaka urais, kuongoza harambee ya kuchangia ujenzi wa msikiti wa Patandi mkoani Arusha Alhamisi wiki hii, ambako habari zinasema siku mbili baadaye huenda mbunge huyo wa Monduli akatangaza rasmi nia yake ya kuanza safari ya kuelekea Ikulu kwa tiketi ya CCM.
Taarifa iliyotolewa jana na mwandishi wa habari wa Makamu wa Rais, Boniface Makene inaeleza kuwa Dk Bilal anakabiliwa na majukumu mengine ya kitaifa na hivyo ametoa ombi maalumu la kuwakilishwa kwenye harambee ya kukamilisha ujenzi wa msikiti huo ulioanza mwishoni mwa miaka 90.
“Makamu wa Rais ameona kuwa shughuli hii ya uchangiaji wa ujenzi wa msikiti isisogezwe mbele kumsubiri, bali iendelee kwa kuwa anaamini Lowasa ana uzoefu katika kufaninikisha shughuli za aina hii. Pia mchango wake katika shughuli za harambee katika shughuli ni wa mfano,” inasema taarifa hiyo.
Pia taarifa hiyo ilieleza kuwa mchango wa wanajamii wanaoswali katika msikiti wa Patandi ni mkubwa kwani wamekuwa wakijitoa kwa namna nyingi kujenga mshikamano baina ya jamii zinazowazunguka bila kuwa na vikwazo na wameshiriki kuwasaidia watoto yatima.
Uamuzi huo wa Dk Bilal, ambaye kwa nafasi yake anaingia kwenye vikao vyote vya juu vya chama tawala, vikiwamo vya Zanzibar, utakuwa umetikisa harakati za kudhibiti baadhi ya makada wanaotajwa kuwania urais, hasa kambi ya Lowassa ambayo inasemekana inalalamikia kuchezewa rafu na uongozi wa CCM, ingawa haijabainisha rafu hizo.
Lowassa ni mmoja wa makada sita waliopewa onyo kali na CCM Februari mwaka jana, likiwazuia kujihusisha na uchaguzi kwa zaidi ya miezi 12 baada ya kubainika kuwa walianza kampeni mapema kwa kushiriki vitendo vinavyokiuka maadili, zikiwamo za harambee na hivyo kutakiwa kuomba kibali kabla ya kushiriki.
Hata hivyo, wiki mbili zilizopita Lowassa na makada wengine wanaotajwa kuwania urais walialikwa Zanzibar kwenye harambee ya kuchangia mfuko wa maendeleo wa mkoa mpya wa Magharibi, ikiwa ni mara ya kwanza kushiriki tangu walipofungiwa na chama hicho mwaka jana.
Wasomi waliotafutwa na Mwananchi kuzungumzia uteuzi huo walikuwa na maoni tofauti.
“Sina mengi, hakuna atakayeshindwa kuona kuwa wana mu-endorse (wanamuunga mkono) huyo. Yeye (Lowassa) ni miongoni mwa watu wanaotajwa kuwania urais, kwa hiyo hii ni moja  ya ‘technic’ mbinu,” alisema Profesa Tolly Mbwete ambaye ni mkuu wa Chuo Kikuu Huria.
Alisema uteuzi huo ni miongoni mwa harakati za kumuweka vizuri Lowassa katika uchaguzi ujao.
Lakini mhadhiri wa sayansi ya siasa wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dk Alexander Makulilo alisema iwapo Lowassa amepewa jukumu hilo na Dk Bilal, maana yake ameonekana ana uzoefu na anaifahamu kazi hiyo na aangaliwe kama waziri mkuu mstaafu na si vinginevyo.

Imehaririwa na;- poatel Africa

Habari yako! Endelea kutembelea Tovuti ya TeknoTaarifa kwa Taarifa murwa za Teknolojia kutoka ndani na nje ya Tanzania, Tupo kwa ajili ya wapenzi wa Teknolojia.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post