Header ads

Header ads
» » MAONI YANGU: ubunifu unaitajika zaidi kuboresha Maonyesho ya Sabasaba

 


 Maonyesho ya 39 ya Kimataifa ya Biashara ya Dar es Salaam, ambayo yalifunguliwa  na Rais Jakaya Kikwete yaliyo sherekewa jana katika viwanja vya Sabasaba hapa jijini katika hali ambayo naweza kusema ni ya kusuasua. Kwa miaka ya hivi karibuni, maonyesho hayo yamekuwa yakikosa msisimko kinyume na ilivyokuwa miongo kadhaa iliyopita, ambapo wananchi wengi walikuwa wakihamasika na kuhudhuria maonyesho hayo,

Ni vigumu kujua mazingira yaliyosababisha kuwapo kwa hali hiyo ya kusikitisha, lakini moja ya sababu zinazotajwa na wataalamu wa masuala ya biashara ni kwamba mamlaka husika zimekosa ubunifu, hivyo zinafanya shughuli hizo kwa mazoea tu. Tatizo ni kwamba zimeweka msisitizo kwenye takwimu zinazoonyesha kwamba mashirika na makampuni yanayoshiriki kwenye maonyesho hayo yanaongezeka, pasipo kufanya tathmini jadidi kuhusu kuongezeka au kushuka kwa viwango na ubora wa ushiriki huo.

Ni kweli kwamba maonyesho ya mwaka huu yamedorora kwa sababu nyingi za msingi. Bunge la Bajeti linaendelea mjini Dodoma, ambapo wabunge, watumishi wa Serikali na taasisi zake wameelekeza vipaumbele vyao kwenye shughuli za Bunge. Pia mwaka huu ni wa uchaguzi na ndiyo maana tunashuhudia jinsi wanasiasa na wafuasi wao kote nchini wanavyozunguka kila kona ya nchi kusaka watu wa kuwaunga mkono, wakiwamo wanaotaka kugombea urais, ubunge na udiwani.
Maonyesho hayo pia yameangukia katika mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani, ambapo ni vigumu kwa waumini wengi wa Kiislam waliofunga kushiriki katika maonyesho hayo kutokana na kuingiliana kwa shughuli hizo.
Pamoja na hayo yote, bado tunadhani mamlaka zinazohusika na maonyesho hayo hazijafanya juhudi za kutosha, kwani zimeshindwa kutambua kwamba maonyesho hayo yanahitaji matayarisho na uhamasishaji mkubwa. Matokeo ya kutotambua hilo ni ukimya kutanda kila mahali kama vile tukio hilo muhimu la kimataifa halifanyiki hapa nchini. Vyombo vingi vya habari viko kimya kuhusu nini hasa kinaendelea katika maonyesho hayo na inashangaza kuona mamlaka husika hazijashtukia hali hiyo. Tovuti husika hazina maelezo ya msingi kuhusu maonyesho hayo, ambayo baadhi ya watu wameyapa jina la ‘gulio la mwaka’.
Mamlaka husika zinapaswa kutambua kwamba kadri miaka inavyopita zinapaswa kubadili mbinu, mifumo na mikakati ya kuendesha maonyesho hayo, kwani mazingira na mahitaji yaliyokuwapo zamani sasa yamebadilika kwa kiasi kikubwa. Huko mwanzo nchi yetu haikuwa na bidhaa muhimu, hivyo wananchi walikuwa wakisubiri maonyesho hayo kwa hamu kubwa ili wanunue bidhaa adimu, ikiwa pamoja na sabuni, mafuta ya kupikia na kadhalika. Wengine walisubiri maonyesho hayo ili kunywa bia kwa sababu kulikuwapo na uhaba mkubwa wa bidhaa hiyo.
Sasa bidhaa hizo na nyingine zipo kwa wingi. Zinahitajika mbinu mpya za kuwavutia wananchi. Mbinu hizo zilenge kufungua fursa za kibiashara kama kutafuta wabia na wawekezaji wa ndani na nje. Maonyesho hayo yalete bidhaa za viwango vya kimataifa ili wazalishaji wa ndani waige namna ya kuvifikia, lakini katika kufanya hivyo lazima kwanza mahitaji ya soko yazingatiwe. Ni matumaini yetu kwamba maonyesho ya mwaka ujao yatakuwa tofauti na miaka iliyopita siyo tu kwa kuwahamasisha na kuwashirikisha wananchi wengi, bali pia kuonyesha bidhaa zilizosheheni ubunifu na vipaji.

Imehaririwa na;- poatel Africa

Habari yako! Endelea kutembelea Tovuti ya TeknoTaarifa kwa Taarifa murwa za Teknolojia kutoka ndani na nje ya Tanzania, Tupo kwa ajili ya wapenzi wa Teknolojia.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post