Header ads

Header ads
» » Fahamu Jinsi ya Kukabiliana na Mwanga wa Vifaa vya Kieletroniki



TAKRIBAN watu milioni 30 nchini Tanzania wanatumia simu za viganjani na haiwezi kupita siku bila kuangalia vioo vya simu zao, iwe ni kuchapa ujumbe wa maneno, kusoma ujumbe wa maneno na video na wengi hutumia mitandao ya simu zao kusoma na kuangalia habari mbalimbali.
Fikiria unachofanya asubuhi punde tu baada ya kushtuka usingizini, pengine uko kama mimi. Kabla hata sijatoka kitandani hujitahidi kusoma barua pepe zote na kujibu jumbe zote nilitumiwa wakati niko usingizini. Na kwa wengine huelekea kazini ambako muda mwingi hutumia kompyuta na vifaa vingine vya kieletroniki vyenye uwezo kama kompyuta.

Wengi tunapenda kutumia vifaa hivi ingawa ni hatari, hivyo tunapaswa kuchukua tahadhari na kulinda macho yetu kama tunavyoyalinda dhidi ya jua. Ukweli ni kwamba vifaa hivi vya kieletroniki vinatoa mwanga hatari wa bluu ambao huathiri kuona na afya kwa ujumla.
Kuendelea kutazama kioo cha kifaa cha kieletroniki kunaathiri macho kwa njia kuu mbili:- 

1. Njia ya kwanza hufanya mtu kukodoa macho kwa muda mrefu bila kukonyeza, kitaalamu hujulikana kama 'Digital Eye Strain.' Tunapoangalia sana kioo kiwango cha kukonyeza hupungua sana na kusababisha matatizo katika macho. Ikiwa umewahi kupatwa na maluelue baada ya kuangalia kompyuta siku nzima, hiyo inaweza kuwa ni ishara ya kuwepo kwa tatizo hili. Wakati mwingine unaweza kuhisi maumivu ya kichwa, macho kukauka au kuhisi macho kuchoka baada ya kuangalia kurasa zako za mitandao ya kijamii. Dalili hizi ni za kawaida sana ingawa watu wengi hawazizingatii. Tatizo la kukodoa bila kukonyeza ni la muda mfupi ingawa likiachwa bila kushughulikiwa kwa muda mrefu linaweza kuwa sugu. 
_14A0687
Njia nyepesi ya kushughulikia tatizo hili ni kukonyeza zaidi. Kukonyeza mara kwa mara kunasaidia jicho kutokauka. Njia nyingine nzuri kuepuka tatizo hili ni kufuata kanuni ya 20-20-20 inayomaanisha kila baada ya dakika 20 angalia kitu kingine kilicho umbali wa angalau futi 20 kwa angalau sekunde 20. Zoezi hili hufanya macho kuwa katika hali ya kawaida tena. Pia, unaweza kupumzika kwa muda mfupi kama unafanya kazi za kompyuta. Jaribu kupumzika kwa dakika 15 kila baada ya saa mbili, pumzisha macho yako kila baada ya dakika 20 kwa kuangalia mazingira ya mahali ulipo. Pia, weka mwanga wa kutosha mahali ulipo wakati unatumia vifaa vya kieletroniki kama kompyuta na televisheni/luninga. Kuangalia kifaa cha kieletroniki gizani au sehemu yenye mwanga mdogo kunafanya macho kufanya kazi ya ziada na mara nyingi husababisha tatizo la kukodoa bila kukonyeza (Digital Eye Strain).
2. Njia ya pili, ambayo matumizi ya vifaa vya kieletroniki huathiri macho yetu ni athari ya mwanga wa bluu kwenye macho. Unaitwa mwanga wa bluu kwa sababu ndio unaosababisha rangi ya bluu kuonekana. Mwanga wa bluu ni hatari kwa kuwa ndio mwanga wenye wimbi kubwa la mwanga. Mwanga huu una nguvu ya kupenya kwenye jicho hadi sehemu ya nyuma ya jicho, njia ya asili ya jicho kuchuja mwanga huu hushindwa kuuzuia mwanga huo na hilo ndio tatizo. Ingawa mwanga wa bluu sio mgeni kwa watu wote, ila kiwango huongezeka pale tunapotumia sana vifaa vya kieletroniki. Jinsi tunavyoendelea kutumia vifaa hivi ndivyo tunavyoongeza athari kwenye macho yetu. Tofauti na tatizo la kwanza la kukodoa bila kukonyeza, mwanga wa bluu husababisha magonjwa ya macho kama madoa kwenye retina (Macular Degeneration) ambavyo humfanya mtu kutoona vizuri.
Watoto nao wapo katika hatari kubwa ya kuathiriwa na mwanga wa bluu kwa kuwa wanaanza kutumia vifaa vya kieletroniki wakiwa wadogo sana. Tofauti kubwa ya macho ya mtoto na mkubwa ni kwamba macho ya mtoto bado hayajapata uwezo wa kuzuia mwanga wowote utakaoathiri macho. Hata hivyo, watu wazima ambao hutumia vifaa vya kieletroniki katika kazi zao za kila siku na maisha binafsi wako katika hatari zaidi.
Unaweza kuchukua hatua za kulinda macho yako dhidi ya mwanga wa vifaa vya kieletroniki kwa kupunguza matumizi ya vifaa hivyo, ikiwa utashindwa kujizuia afadhali kabla ya kulala. Tafiti zinaonyesha kuwa matumizi ya vifaa vya kieletroniki kabla ya kulala huharibu usingizi.
Ni vyema kuzungumza na daktari wa macho atakuchagulia lenzi itakayokusaidia kuchuja mwanga wa bluu. Lenzi utakazotumia zitakusaidia kupunguza mwanga kwa muda wote. Wengi waliotumia lenzi hizi waliweza kupumzisha macho yao. Ikiwa una watoto wadogo ni kitu cha busara kuwanunulia miwani yenye lenzi maalumu za kupunguza mwanga hatari.
Weka hali ya hewa nzuri mahali unapotumia kifaa chako cha kieletroniki. Mahali hapo pasiwe na joto au baridi sana pawe na ubaridi wa kawaida na pasiwe na moshi au vitu vingine vinavyochafua hali ya hewa. 

Rejesho: Dk. Joachim Mabula

Imehaririwa na;- Unknown

Habari yako! Endelea kutembelea Tovuti ya TeknoTaarifa kwa Taarifa murwa za Teknolojia kutoka ndani na nje ya Tanzania, Tupo kwa ajili ya wapenzi wa Teknolojia.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post