Shekhe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake.
Shekhe Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Alhad Mussa Salum ametangaza Swala
ya Sikukuu ya Idd El Fitri inayotarajiwa kufanyika kitaifa katika mkoa
wake.
Akizungumza na waandishi wa habari kwenye kikao maalumu katika Ofisi za
Mkoa wa Dar es Salaam za Baraza Kuu la Waislamu (BAKWATA) hii leo,
Shekhe Alhad alisema kuwa swala hiyo sambamba na hotuba mbalimbali
inatarajiwa kufanyika saa moja asubuhi katika Viwanja vya Mnazi Mmoja
jijini Dar kutegemea na siku ya Idd itakapodondokea ambapo inatarajiwa
kuwa siku ya Jumatatu Julai 28 au Jumanne Julai 29 mwaka huu.
Shekhe Alhad alisema kuwa swala hiyo itahudhuriwa na Rais wa Serikali ya
Jamhuri ya Tanzania, Jakaya Kikwete na viongozi mbalimbali wa Kiislamu
na wa kitaifa ikifuatiwa na Baraza la Idd litakalofanyika saa 9 Alasiri
katika Viwanja vya Karimjee, Dar ambapo Mgeni Rasmi wa Baraza hilo
atakuwa ni Waziri Mkuu wa Tanzania, Mizengo Peter Pinda.