Header ads

Header ads
» » Kutana na MZUNGU Anayeuza Mandazi Nchini KENYA

MIAKA tisa iliyopita Terry Dean Baucom alikuwa muuzaji wa magazeti katika barabara za Jimbo la Michigan nchini Amerika. Lakini kwa sasa, Bw Baucom mwenye umri wa miaka 49 ni muuzaji wa mandazi katika mitaa ya mji wa Siaya, eneo la Nyanza.
Kwa siku tano kwa wiki, Bw Baucom huchuuza mandazi na bisi (mahindi yaliyokaangwa) akitumia baiskeli.
Tangu alipowasili Siaya mnamo Agosti 2014 pamoja na mkewe na binti zake watatu, Bw Baucom amejifunza lugha ya Kidholuo na ana uwezo wa kuzungumza lugha hiyo japo maneno kadhaa humtatiza.
“Amosi (hali gani?)” aliamkua waandishi wa Taifa Leo wakati walipokutana naye ili kumhoji.
Bw Baucom na familia yake wanaishi katika mtaa wa Banana viungani mwa mji wa Siaya. Alisema kuwa alijitosa katika biashara ya kuchuuza bidhaa hizi kama njia nzuri ya kuwashawishi wakazi wa Siaya kusaka na kupata fedha za kusaidia wasiojiweza.
Bw Baucom huuza mandazi, bisi na keki katika maduka ya jumla na yale madogo madogo.
Wakazi wa Siaya wanasema kuwa keki anazotengeneza Baucom ni za kipekee kwani huwa na ladha tofauti tofauti kama vile 'vanila’ na ndizi.
“Nilianza kazi hii kwa sababu wasio na chochote katika jamii wamepuuzwa na matajiri, kando na kutoheshimiwa na wengi,” akasema Bw Baucom.
mzungu-pic
Alisema hufanya biashara hiyo kwa madhumuni ya kusaidia watu maskini katika kanisa lake la New Covenant Outreach World ambalo lina makao makuu nchini Amerika.
Bw Baucom alisema wenyeji wa eneo hilo wanashangaa kuona raia wa Amerika akijihusisha na uchuuzi lakini azma yake ya kusaidia wasiojiweza humpa motisha kila siku.
Kuhubiria watu
“Japo biashara hii haina faidi kubwa, ninapata mapato ya kutosha kukimu mahitaji ya familia yangu na pia kusaidia maskini katika jamii,” aelezea Bw Baucom.
Anapowauzia wateja wake bidhaa hizi, Bw Baucom, vilevile, huwahubiria mafunzo ya Kikristo.
“Kama Mkristo, ni muhimu kuwa na moyo mkunjufu. Natumia biashara yangu kuinua kanisa na kuwapa moyo maskini pamoja na kufadhili elimu ya watoto mayatima mjini Siaya,” akaeleza.
Bw Baucom alisema kuwa kwa siku anapata faida ya Sh2, 000 na kati ya fedha hizo, hutoa Sh500 kwa shughuli za kanisa hilo la New Covenant Outreach lililoko katika barabara ya Siaya-Ndere.
“Huwa ninatoa kati ya Sh300 hadi 500 kila siku kwa shughuli za kanisa kulingana na faidi ambayo nimepata kwa siku,” alieleza Bw Baucom.
Kwa usaidizi wa binti zake na mkewe, amefanikiwa kuongeza mapato yake kwa sababu wanasambaza bidhaa zake kwa wateja zaidi.
Katika siku za wikendi, familia ya Bw Baucom hutembelea wafungwa katika jela ya Siaya na wagonjwa katika Hospitali Kuu ya Kaunti ya Siaya, kuwafanyia maombi.
Bw Baucom alizaliwa katika Jimbo la Michigan na akahamia Ufilipino mnamo 1997 baada ya kuacha kazi yake ya kuuza magazeti.
Alianzisha kanisa la New Covenant Outreach World mnamo 2009 na akatumwa Kenya mnamo Agosti 2014.

Imehaririwa na;- poatel Africa

Habari yako! Endelea kutembelea Tovuti ya TeknoTaarifa kwa Taarifa murwa za Teknolojia kutoka ndani na nje ya Tanzania, Tupo kwa ajili ya wapenzi wa Teknolojia.
«
Next
Newer Post
»
Previous
Older Post